Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), anayeshughulikia Afya, Dkt. Jafar Seif, amewasili Makete na kukagua ujenzi wa majengo sita katika kituo cha afya Lupalilo kilichopandishwa hadhi kutoka zahanati ya Kijiji, ambapo ujenzi huo uliogharimu Shilingi Milioni 580.2 utawezesha kupunguza idadi ya rufaa za wagonjwa ambazo zilikuwa zikiwaongezea wananchi gharama za matibabu.
Akiwahutubia wakazi wa Lupalilo leo Dkt. Seif amesema dhamira ya Serikali ni kupunguza rufaa hasa kwa maeneo ya vijijini kwa kuboresha huduma za afya ngazi ya msingi ili kuhakikisha wananchi wa maeneo ya pembezoni wanahudumiwa vizuri kama ilivyo kwa maeneo ya mijini.
Majengo yote sita(6) yaliyokaguliwa na Dkt. Seif, ni pamoja na la Wagonjwa wa Nje (OPD), huduma za Wazazi, Maabara, Upasuaji, jengo la kufulia na kichomea taka ambayo yote yamekamilika na yanaendelea kupokea vifaa tiba kutoka Bohari ya Dawa (MSD) vyenye thamani ya Shilingi Milioni 300.
Kwa upande wake, Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Lupalilo, Odetha Mutyaba, amesema kwamba kukamilika kwa kituo hicho kumeboresha utoaji wa huduma za wagonjwa kutoka wagonjwa 541 hadi wagonjwa 1,903 kwa mwaka 2025, ambapo hatua hiyo imechangia ongezeko la mapato kutoka Shilingi 150,000 hadi 500,000 kwa mwezi.
1 CDA Street, 40477
Anuani ya posta: 1249, DODOMA, TANZANIA
Simu: +255 26 232 4817
Simu ya kiganjani:
Baruapepe: cd@dodomacc.go.tz
Copyright ©2017 The City Council of Dodoma. All rights reserved.